Shein: Ni ukatili
Padre Mwang`amba ahamishiwa Muhimbili
Aliyemmwagia tindikali kupatikana kirahisi
Aliyemmwagia tindikali kupatikana kirahisi
Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein
Dk. Shein alitoa agizo hilo jana katika
Hospitali ya Mnazi Mmoja mjini Unguja, alipokwenda kumjulia hali Padre
Anselmo Mwang’amba wa Kanisa Katoliki, parokia ya Machui, aliyemwagiwa
maji yanayosadikiwa kuwa tindikali, juzi jioni.
“Hatuwezi kuviacha vitendo hivi
viendelee...ni lazima jeshi la Polisi lijitahidi kuwatafuta wahusika ili
sheria ichukue mkondo wake,” alisema.
Amekiita kitendo hicho kuwa ni cha
kikatili na kisichovumilika na kuongeza kuwa wahusika lazima wasakwe na
kuchukuliwa hatua za kisheria.
Dk. Shein, alielezea kusikitishwa na
kitendo hicho na kumpa pole Padre Mwang’amba na kumuomba Mwenyezi Mungu
ampe nafuu haraka apone ili aendelee kuitumikia jamii.
Akizungumza na waumini wa kanisa hilo nje
ya wodi hiyo, Dk. Shein, aliwataka waumini hao kuwa na subira wakati
serikali ikichukua hatua kukabiliana na kitendo hicho.
“Ni jambo la kusikitisha kumfikisha
binadamu mwenzako katika hali kama hii ya majonzi. Hakuna anayeyataka
haya. Tuwe wastamilivu serikali tunachukua hatua,” aliwaambia waumini
hao.
Akizungumzia hali yake, Padre Mwang’amba
alimueleza Rais kuwa ni nzuri, lakini anatarajia kupata nafuu zaidi
baada ya uvimbe kupungua sehemu za machoni.
“Hali yangu ni nzuri lakini natarajia
uvimbe ukipungua nitaona vizuri zaidi” alisema Padri Mwang’amba na
kuongeza kuwa ilikuwa ni bahati kwake hakuathirika sana.
Alisema tukio hilo lilitokea eneo la
Mlandege jioni, wakati akitoka katika ofisi moja inayotoa huduma za
`intaneti’ katika eneo hilo ndipo akatokea kijana mmoja na kumwagia
tindikali.
Wakati huo huo Katibu Mkuu wa Wizara ya
Afya, Dk. Mohamed Saleh Jidawi, akiwa amefuatana na Mkurugenzi wa
Hospitali hiyo, Dk. Jamala Adam Taibu, amesema alipofikishwa katika
hospitali hiyo, Padre Mwang’amba alipatiwa huduma zote muhimu .
Kuhusu majeraha aliyopata, Dk. Jidawi
alisema kuwa kwa ujumla asilimia 30 ya mwili wake (Padre Mwang’amba)
umeathirika na kidogo sehemu za macho.
Padre Mwang'amba, amehamishiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi.
Padre Mwang'amba alifikishwa hospitalini hapo majira ya saa 4:00 asubuhi akitokea Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja, Zanzibar.
Alisafirishwa kwa ndege iliyokodiwa na
Kanisa Katoliki nchini, ambapo aliwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa
Julius Nyerere majira ya saa 3.30 asubuhi na kupelekwa moja kwa moja
kwenye wodi ya wagonjwa wa dharura kwa ajili ya uchunguzi.
Akizungumza mara baada ya kufikishwa wodi
namba 10 jengo la Kibasila, Padre Mwang'amba alisema hali yake
inaendelea vizuri, madaktari wanaendelea kumpatia tiba. "Nashukuru hali
yangu inakwenda vizuri, nimewasili leo (jana) madaktari wanaendelea
kunitibu," alisema.
Hata hivyo, hakutaka kuongeza zaidi na kuomba aachwe ili apumzike.
Mkuu wa wauguzi wa jengo hilo, Ruthi Rutabingwa, alisema amempokea mgonjwa huyo na jitihada za kitabibu zinaendelea kufanywa.
"Nathibitisha kumpokea mgonjwa akiwa katika hali ya kuridhisha," alisema Rutabingwa.
Katika hatua nyingine, mmoja wa watu
walioambatana naye kutoka Zanzibar, ambaye hakutaja jina lake litajwe,
alisema mtu aliyefanya tukio hilo anaweza kujulikana haraka kutokana na
nyumba aliyokimbilia kujificha kufahamika.
Alisema, mtu aliyemmwagia tindikali
kiongozi huyo wa kidini, mara baada ya tukio hilo alikimbilia kwenye
nyumba moja jirani na eneo hilo na baadhi ya watu walimuona.
"Kama polisi itakuwa makini, kazi ya
kumpata yule kijana itakuwa rahisi kwa sababu baada ya kummwagia padre
tindikali alikimbilia kwenye nyumba moja," alisema.
Alisema wakati wanakuja Dar es Salaam, amesikia watu wanaoishi kwenye nyumba hiyo wamekamatwa kwa mahojiano.
CHANZO:
NIPASHE JUMAPILI
duuuuh
ReplyDelete