Wachezaji ligi kuu kupimwa mkojo
Wachezaji
wa ligi kuu ya Bara watakuwa wakipimwa mkojo kwa kushitukizwa kila
baada ya mechi katika msimu ujao ili kubaini wenye kujihusisha na
matumizi ya madawa yaliyopigwa marufuku, imeelezwa.
Akizungumza jijini mwishoni mwa wiki,
msemaji wa shirikisho la soka, TFF, Boniface Wambura alimsema wachezaji
watakuwa wakichaguliwa bila utaratibu maalumu kila baada ya mechi kwa
ajili ya kuchukuliwa sampuli za kufanyiwa vipimo.
Ligi kuu ya Bara itaanza Agosti 24 kwa
mechi saba zitakazozikutanisha Yanga na Ashanti, Mtibwa Sugar na Azam,
JKT Oljoro na Coastal Union, Mgambo JKT na JKT Ruvu, Rhino Rangers na
Simba, Mbeya City na Kagera Sugar, na Ruvu Shooting dhidi ya Prisons.
Wambura alisema jopo la madaktari wa TFF
kwa kushirikiana na tabibu wa klabu husika watachagua wachezaji bila
mpangilio maalumu katika mechi mbalimbali za ligi.
Wachezaji watakaochaguliwa, alisema Wambura, watachukuliwa sampuli ya mkojo kwa ajili ya uchunguzi wa maabara.
Wote watakaobainika kutumia madawa
yaliyopigwa marufuku michezoni, alisema Wambura, watafungiwa kwa mujibu
wa kanuni zinazosimamia kosa hilo.
“Utumiaji madawa yaliyopigwa marufuku ni
tatizo la dunia nzima, na kwa Tanzania pia tunayapiga vita kwa sababu
yanaondoa ushindani wa haki kwenye michezo," alisema Wambura.
“Hapa nchini wachezaji wengi ambao
wanatumia madawa yaliyopigwa marufuku hujihusisha na uvutaji wa bangi
ambayo ni vigumu kuigundua mwilini mwa mchezaji ambaye alitumia miaka
miwili au mitatu iliyopita, hivyo inahitaji kuchunguzwa kwa muda mrefu.
“Lakini TFF itaendelea kuipiga vita na nina hakika tutapunguza uvutaji bangi huu kama si kuutokomeza kabisa."

Wambura aliwataka wachezaji na viongozi wa
klabu kuungana na TFF na FIFA, shirikisho la soka la kimataifa, kupiga
vita matumizi ya madawa haramu ili kuinua ushindani wa haki kwenye
mchezo huo.
Msemaji huyo wa TFF alisema shirikisho
linakusudia kuwekeza zaidi kwenye elimu juu ya madhara ya madawa haramu
kwenye michezo, hata hivyo, na kueleza jina la Tanzania bado ni safi
katika anga ya kimataifa.
“Timu ya taifa imecheza zaidi ya mechi 10
(katika miaka miwili iliyopita), Azam na Simba zimeshiriki michuano ya
klabu ya Afrika (mwaka huu) lakini hakuna mchezaji aliyegundulika
kutumia madawa," alisema Wambura.
Wambura alisema katika michuano ya
kimataifa maofisa wa FIFA na wa CAF, shirikisho la soka la Afrika,
hufanya pia uchunguzi wa madawa haramu kwa kushitukiza mara kwa mara.
CHANZO:
NIPASHE JUMAPILI
0 comments: